Friday, March 15, 2013

PAPA FRANCIS, AFANYA MAAJABU AMBAYO WATU WENGI HAWAKUTEGEMEA.....SOMA ALICHOKIFANYA SIKU YAKE YA KWANZA TU


 

VATCAN-ITALIA,
PAPA Francis I ameonesha maajabu katika siku yake ya kwanza ya upapa, baada ya jana kwenda katika hoteli aliyofikia kabla ya kuchaguliwa kuwa Papa wa 266 katika historia ya Kanisa Katoliki duniani, kuchukua mizigo yake na kulipa bili yeye mwenyewe.

Hali hiyo, iliashiria kuachana na staili za watangulizi wake, ambao wamezoea kufanyiwa shughuli kama hizo na watumishi wao, huku wenyewe wakijifungia ndani ya nyumba za gharama ambazo kuta zake zimenakishiwa kwa dhahabu za mjini Vatican.

Jambo la pili ambalo lilionekana kuwavutia wengi, ni pale alipoachana tena na desturi za mapapa waliopita, uchaguzi wa mavazi ya kipapa ya Francis I ulijidhihirisha kwa kuvalia vazi la kawaida lisilotofautiana na lile la zama zake za uaskofu.

Askofu huyo wa zamani wa Buenos Aires, Argentina, Kardinali Jorge Bergoglio, alianza siku yake ya kwanza kwa kufanya ziara kwa kutumia gari la kawaida la Vatican kuelekea Basilica la Roman ili kufanya maombi kwa Bikira Maria, akilenga kulileta kanisa karibu na watu.

Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 76, alihudhuria misa ya maombi katika Kanisa la Santa Maria Maggiore mjini Roma, ili kuanza kazi yake kama mkuu wa Wakatoliki bilioni 1.2 kote duniani.

Papa huyo wa kwanza kutoka Amerika ya Kusini, alipokea ujumbe na salamu mbalimbali kutoka duniani kote kumtakia heri.

Miongoni mwao, ni Rais wa Marekani, Barack Obama, aliyemtaja Bergoglio kuwa mtetezi wa masikini na wanyonge, huku Makamu wake, Joe Biden akitarajia kuongoza ujumbe wa nchi hiyo katika sherehe za kumsimika zitakazofanyika Jumanne wiki ijayo.

Aidha Waziri Mkuu wa Australia, Julia Gillard, alisema kuchaguliwa Papa kutoka ‘ulimwengu mpya’ ni tukio ambalo lina umuhimu wa kihistoria.

Viongozi wengine, waliotuma pongezi ni pamoja na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon na Rais wa Argentina, Cristina Kirchner.

Francis, ambaye ndiye Papa wa kwanza asiyetoka Ulaya katika kipindi cha takribani miaka 1,300, aliitumia ibada yake ya kwanza kumwombea mtangulizi wake, Benedict VXI na kutoa wito wa kuwepo udugu miongoni mwa waumini wa Kikatoliki.

Lakini Muargentina huyo, pia anakabiliwa na mlolongo wa changamoto ngumu zinazolikabili kanisa hilo.

Kanisa hilo, limekumbwa na migawanyiko mikubwa ya ndani na kashfa zilizowakumba makasisi za kuwadhalilisha watoto kingono na tuhuma za ufisadi na kuvuja kwa nyaraka za siri.

Awali alikuwa ameuambia umati wa watu 100,000 uliofurika katika kiwanja cha Mtakatifu Petro kwamba amepanga kumwomba Bikira Maria ili auangalie mji mzima wa Rome.

Aliwaambia makardinali kwamba atamtembelea Papa mstaafu Benedict XVI, lakini Vatican ilisema ziara hiyo itafanyika siku chache zijazo.

Ratiba kuu ya Papa Francis I, jana ilikuwa kuzindua ibada ya jioni katika Kanisa dogo la Sistina, ambako makardinali juzi usiku walimchagua kuwa kiongozi wa kanisa hilo lenye waumini bilioni 1.2.

Anatarajia kutumia zaidi Kiitaliano na kuachana na utamaduni wa Benedict ambaye alijikita zaidi katika Kilatini.

Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 76, anayesemekana kushika nafasi ya pili nyuma ya Papa Benedict XVI alipochaguliwa mwaka 2005, alichaguliwa katika raundi ya tano kumrithi papa huyo wa kwanza kujiuzulu kipindi cha miaka 600.
MWARICK JAPHET TEKELE MUJUNGU Web Developer

ASANTE KWA KUTEMBELEA KING SELE BLOG KWA MSAADA ZAIDI WASILIANA NASI: E-mail.: mwarickit@gmail.com.

No comments:

Post a Comment