Thursday, July 26, 2012

Ukiona dalili hizi 20 kwa mkeo, bora umuache tu!


TUKO kwenye Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, niwape pole wale waliojaaliwa kufunga na niwasihi wale wenye uwezo huo wafanye hivyo ili kumfurahisha Mwenyezi Mungu aliyetuumba.
Lakini nitoe angalizo kwa wale wenzangu na mimi wasiofunga, wajitahidi kutowaharibia swaumu wenzao. Wewe msichana uliyezoea kuvaa kimitego hebu funga breki kipindi hiki ili kutowatia majaribuni wenzako.
Aidha, kama wewe una mpenzi wako ambaye ni Muislam na wewe ni Mkristo, iheshimu imani yake na ikiwezekana mpe sapoti ili aweze kuvuka kipindi hiki salama.
Ndugu zangu, mmoja wa wadau wakubwa wa safu hii aliyejitambulisha kwa jina la Jafari wa Arusha, ameuliza swali ambalo nimeona ni vyema nikamjibu kupitia hapa ili na wengine waweze kufaidika
.
Yeye alitaka kujua jinsi anavyoweza kumbaini mwanamke asiye na mapenzi ya dhati kwa mumewe. Katika kujibu hili nimeorodhesha dalili 20 ambazo ukiziona kwa mpenzi wako ni bora ukamuacha tu.
Moja, Ni mwepesi wa kuanika udhaifu wako kwa watu wengine, ni mgumu wa kukusifia mbele za wenzake badala yake haoni noma kukuponda.
Mbili, anakuwa mgumu sana kukutambulisha kwa rafiki zake na ndugu.
Tatu, haonyeshi kubana matumizi kwa ajili ya maendeleo, kwake ni kufuja mali na anapokosa kupewa fedha ni mwepesi kulalamika.
Nne, anaahirisha mara kwa mara kukutana na wewe tena bila kukueleza sababu za msingi. 
Tano, anapokuwa anatoa maelezo ya mwanaume anayempenda kwenye maisha yake, sifa zake zinakuwa si zile ulizonazo wewe.
Sita, si mtu wa kucheka kwa furaha, hata kama ukimchekesha haoneshi furaha ya moyoni, tena mara nyingine anakuwa mkimya.
Saba, anajaribu kukuunganisha na wanawake wengine, haoni vibaya anaposikia unamfukuzia hata rafike yake badala yake anaweza hata kukutia moyo. Kwa kifupi hana wivu na wewe.
Nane, haumii pale inapotokea amekukosea, ni mwepesi wa kujitenga, kutozungumza na wewe na mwingi wa kukusukumia makosa hata kama yeye ndiye aliyekukosea.
Tisa, hataki kuambatana na wewe katika matembezi na ikitokea anakuwa mtu wa masharti sana. Ni rahisi kukuambia utangulie, yeye anakuja au mnaweza kutoka pamoja lakini yeye akawa anatembea mbali na wewe.
Kumi, siku zote ni mtu wa kupokea tu na si wa kutoa. Analazimisha kukumbatia mali zako na zake pia. Hupenda kufanya mambo yake kwa siri lakini hulazimisha kujua mipango yako.
Kumi na moja, hakumis hata unapokuwa mbali naye, kwa kifupi hathamini uwepo wako na anakuchukulia kama mtu wa akiba kwake.
Kumi na mbili, hakupi moyo pale unaposhindwa katika mambo unayopanga. Hachukui huzuni yako kama yake, hakufariji na hakusaidii pale ulipokwama.
Kumi na tatu, anayeweza kuchochea hisia mbaya kwa watu ili jamii ikuone mbaya, unayestahili kudharauliwa. Anakuwa mstari wa mbele kukuchafua katika maeneo ambayo anastahili kukusafisha.
Kumi na nne, hakupi kipaumbele katika maamuzi, anajiona yeye ndiye wa kwanza na wewe ni mtu wa kufuatia.
Kumi na tano, muwapo faragha anafanya bora liende, hakufikishi pale ambapo ulitarajia. Kwa kifupi anakuwa hana msisimko na wewe.
Kumi na sita, hakuhudumii tendo la ndoa mpaka siku amependa yeye. Ni mwingi wa kutoa sababu za kuchoka, kusingizia ugonjwa.
Kumi na saba, hazungumzii maendeleo yenu, ni mtu anayependa kufikiria maendeleo binafsi na ikiwezekana kuuza vilivyopo ili atimize malengo yake.
Kumi na nane, hataki kuambiwa ukweli na inapotokea akaambiwa huwa mkali na kuja juu mithili ya moto wa kifuu.
Kumi na tisa, hata akukosee vipi ni mgumu wa kuomba samahani na ikitokea umekosea wewe, ni mgumu kukusamehe kiasi kwamba kosa la mwaka jana anaweza kulikumbushia leo.
Ishirini, haoni hatari kukuambia; ‘Kama vipi tuachane, kwani nini....? Wapo wanaume wengi na wananitaka’.
MWARICK JAPHET TEKELE MUJUNGU Web Developer

ASANTE KWA KUTEMBELEA KING SELE BLOG KWA MSAADA ZAIDI WASILIANA NASI: E-mail.: mwarickit@gmail.com.

No comments:

Post a Comment