Saturday, December 1, 2012

CHEKI BAADHI YA MALI ZA SHARO MILLIONEA ZILIZOPATIKANA MPAKA SASA




 Baadhi ya vitu vya marehemu Sharo milionea 
vilivyokamatwa baada ya msako mkali baina 
ya Polisi na wananchi wa Kijiji Songa Kibaoni.
WATU wanaosadikiwa kuiba vitu vya marehemu 
Hussein Mkiety maarufu kwa jina la 'Sharo Milionea' 
aliyefariki kwa ajali ya gari katika kijiji cha Songa 
Kibaoni wilayani Muheza Novemba 26 mwaka huu, 
wamesalimisha baadhi ya vitu hivyo kwa 
mwenyekiti wa Kijiji hicho huku wakiendelea
 kuishi mafichoni kuogopa kutiwa mbaroni.

Watu hao wamesalimisha vitu hivyo baada ya
 Mkuu wa wilaya ya Muheza Subira Mgalu
 ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya 
ulinzi na usalama kuwatangazia kwamba wale
 wote waliomwibia marehemu watasakwa na
 kuchukuliwa hatua za kisheria kufutia kitendo
 walichokifanya kutokuwa cha kiungwana.

Mkuu huyo pamoja na jeshi la polisi wilayani humo
 waliendesha msako juzi usiku lakini hawakuweza 
kuwakuta watu baada ya kuzihama nyumba zao
 kuogopa kutiwa mbaroni na mkuu huyo
 kuwalazimsha baadhi ya familia walizozikuta 
kuendesha zoezi la kuwataja watu wanaohofiwa 
kwamba huenda watakuwa wamchukua vitu hivyo.

Kamanda wa polisi mkoani Tanga ACP Constatine 
Masawe, aliwaeleza waandishi wa habari ofisini
 kwake kuwa, usiku wa kuamkia juzi mwenyekiti
 wa kijiji hicho Abdi Zawadi alipelekewa vifaa
 mbalimbali ikiwemo nguo ambazo marehemu 
alikuwa amezivaa pamoja na spea tairi ambalo
 waliling'oa na kutokomea porini.

Kamanda huyo alitaja vitu vilivyokabidhiwa kwa 
mwenyekiti huyo kuwa ni pamoja na begi lake
 lililokuwa na 'viwaro' nguo zake, betri ya gari hilo
 lililokuwa na namba T 478 BVR aina ya Toyota Harrier,
 saa yake ya mkononi, simu yake aina ya 
Blackberry na redio ya gari iliyokuwa pia
 imeng'olewa na wezi hao.

Kamanda huyo alisema vitu hivyo vilipelekwa na 
mtu mmoja ambaye kwasasa jeshi hilo linashindwa
 kumtaja jina lake kwa vile alijitambulisha 
kwamba ana undugu na wezi hao ambao walimpa
 vitu hivyo avipeleke kwa uongozi wa kijiji hicho
 hatua ambayo alidai kwamba wanafanya
 uchunguzi ili kuwatia nguvuni wale wote 
waliohusika na tukio hilo.
 
Alisema waliweka mtego baada ya kusikia kwamba
 kuna mwizi mmoja wapo anaitafutia mteja simu ya
 mkononi ya marehemu lakini wakati wameweka
 mtego huo kijana huyo alipokuwa akijadiliana 
bei na mtu waliyemweka, alibaini na alipompa 
mkononi alikimbia vichakani kuogopa kukamatwa.
 
Kamanda huyo aliwashukuru baadhi ya wananchi wa
 kijiji hicho pamoja na Mkuu wa wilaya kuhakikisha
 wanashirikiana na jeshi hilo ili kuwabaini na 
 kuwakamata wote waliohusika katika tukio 
hilo ambalo limetokea huku wananchi kadhaa 
wakiomboleza kifo cha msanii huyo ambaye 
alizikwa kijijini kwao Lusanga wilayani Muheza juzi.

Katika hatua nyingine kamanda huyo alisema katika
 matukio ya ajali yaliyotokea mwezi huu wa Novemba 
jumla ya ajali 10 zilitokea ambazo zimesababisha 
 vifo ni 7 na zilizosababisha watu kujeruhiwa ni tatu, 
kati ya hizo watu 12 walipoteza maisha na wengine 
wanane walijeruhiwa.

Kamanda Masawe alisema jumla ya makosa 2,365 
yalitendeka na kupigwa faini iliyosababisha serikali
 kujiingiza kiasi cha sh. 70,950,000 hatua ambayo 
kamanda huyo alisema haioneshi kwamba watumiaji
 barabara wamekuwa wakifuata wakitii sheria za usalama barabarani.
MWARICK JAPHET TEKELE MUJUNGU Web Developer

ASANTE KWA KUTEMBELEA KING SELE BLOG KWA MSAADA ZAIDI WASILIANA NASI: E-mail.: mwarickit@gmail.com.

No comments:

Post a Comment