Wednesday, September 7, 2016

JPM atoa siku saba kwa wadaiwa sugu NHC


Siku chache baada ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) litoe nje vitu vya mmiliki wa Mbowe Hotels Limited, Freeman Mbowe kwa kile kilichoelezwa kushindwa kulipa kodi ya pango iliyofikia Sh bilioni 1.172 , Rais Dk. John Magufuli amempongeza Mkurugenzi wa Shirika hilo, Nehemia Mchechu kwa hatua hiyo.

Pamoja na hali hiyo ametoa siku saba kufukuzwa kwa wapangaji wote wa NHC watakaoshindwa kulipa kodi ya pango, zikiwemo wizara, taasisi za Serikali, watu binafsi na watumishi wa umma.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika mkutano wake na waliokuwa wakazi wa Magomeni Kota, Rais Dk. Magufuli, alisema hatua zinazochukuliwa na Mchechu zitasaidia upatikanaji wa fedha za kuwekeza kwenye miradi mipya.


“Nakupongeza kwa hatua unazoendelea kuchukua. Wale wapangaji wote ni lazima walipe madeni yao, nimetoa maagizo leo (jana) wapangaji wote wa Serikali, Wizara ya Ujenzi, wizara gani kule ndani ya siku saba lazima wawe wameshalipa madeni yao,” alisema Rais Magufuli na kuongeza:


“Wasipolipa endelea kuwatoa nje kama ulivyomtoa yule jamaa (Mbowe),” alisema na kusababisha watu kushangilia huku wakiangua vicheko.


“Endelea hivyo hivyo usiogope kumtoa nje mtu yeyote. Awe amepangishwa ni wa CCM mtoe nje, awe ni wa Ukawa mtoe nje, awe mtumishi wa Serikali mtoe nje, awe mtumishi huyo ni waziri mtoe nje, awe ni Rais mtoe nje,” alisema Rais Magufuli.


Alisema anashangaa kuona watumishi wa Serikali wakishindwa kulipa madeni ya kodi za pango wakati kila siku wanaomba safari za nje huku wakilipana posho.


“Ukipanga na ukashindwa kulipa kodi jiandae kuondoka. Nataka uendelee kuwatoa na nakueleza kweli Nehemia sitanii ‘take it from me and I am very serious’ (nisikilize mimi sifanyi mzaha) ” alisisitiza.


Alisema madeni hayo yangekusanywa yangelisaidia shirika hilo kuwekeza katika maeneo kama la Magomeni Kota ambalo limekaa kwa muda mrefu bila kuendelezwa.


“Inawezekana ungekuwa na hizo fedha ungeshajenga katika eneo hili kuliko kuanza kumtafuta mwekezaji kwa ujanjaujanja. Haiwezekani eneo kama hili (Magomeni Kota) la ekari 33 unazitoa hivi hivi na ni mali ya Serikali,


“Afadhali umtoe mke wako umpe mzaramo mtani wangu akae naye,” alisema Rais Magufuli huku wananchi wakiangua kicheko.

Alimsisitizia Mchechu kuharakisha kuzitoa wizara zinazodaiwa kwenye majengo yake ili ziharakishe kwenda kujenga Dodoma yaliko makao makuu ya nchi.


Awali Rais Magufuli, alisema alibaini ukweli kuhusu eneo hilo kwamba lilitaka kuuzwa kwa mwekezaji kinyemela na kuwaacha bila kitu wakazi hao.


VIA Mtanzania
MWARICK JAPHET TEKELE MUJUNGU Web Developer

ASANTE KWA KUTEMBELEA KING SELE BLOG KWA MSAADA ZAIDI WASILIANA NASI: E-mail.: mwarickit@gmail.com.

No comments:

Post a Comment